TAPO Logo

TAPO Logo

Sunday, April 11, 2010

Gombe watakiwa kushirikisha wananchi

Leonard Mubali, Kigoma

KAMATI ya Bunge ya Maliasili na Mazingira, imeushauri uongozi wa Hifadhi ya Taifa ya Gombe, mkoani Kigoma, kushirikisha wananchi katika mpango wa upanuzi wa hifadhi hiyo, ili kuepuka migogoro isiyokuwa ya lazima.


Hifadhi hiyo inahitaji eneo zaidi, kwa ajili ya kuboresha ikolojia ya sokwe na upanuzi wa huduma za kitalii.


Ushauri huo ulitolewa juzi na Kaimu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Profesa Raphael Mwalyosi, alipokuwa akichangia hoja kuhusu mpango wa kupanua eneo la hifadhi hiyo.


Profesa Mwalyosi alisema mpango huo ni mzuri, lakini lazima kwanza uongozi wa hifadhi, uwashirikishe wananchi wanaoishi jirani na hifadhi, ili kuepuka migongano kati ya pande hizo mbili.


Alisema vitendo vya kutowashirisha wananchi katika kuchukua maeneo kwa ajili ya upanuzi wa hifadhi, vimesababisha migongano isiyokuwa ya lazima, kama ilivyowahi kutokea katika baadhi ya maeneo hapa nchini.


Alisema kwa msingi huo, kuna haja kwa uongozi wa Hifadhi ya Taifa ya Gombe, kuepuka hilo, ili kuwa katika nafasu mzuri ya kuendeleza uhusiano kati yake na wananchi wanaoishi jirani na hifadhi.


Kwa mujibu wa Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Gombe, Noella Myonga, hifadhi hiyo inaomba kuongeza eneo la kilometa 31, ili hatimaye kuifanya iwe na ukubwa wa kilometa 83 za mraba.


Myonga alisema hata hivyo, eneo linaloombwa si la makazi ya watu na kwamba ni la ufukwe wa Ziwa Tanganyika, ambalo uongozi unaamini kuwa, halitakuwa na mlolongo mrefu kuhusu fidia.


Alisema kuongezwa kwa eneo hilo, kutasaidia kuongeza ikolojia ya hifadhi, vivutio zaidi ya sokwe na kuwafanya watalii kufurahia.


Pia alisema kama eneo hilo litahifadhiwa kikamilifu, usalama wa mazalia ya samaki ambayo kwa sasa, yanaharibiwa na wavuvi, utakuwa mkubwa.


Myonga alisema hatua hiyo pia itasaidia kudhibiti watu wanaoishi karibu na Hifadhi ya Gombe, kupita katika eneo hilo kwa njia za miguu, jambo ambalo ni la hatari kwa maisha ya sokwe, hasa ikizingatiwa kuwa wanaweza kuambikizwa kwa urahisi, magonjwa ya binadamu.


Kuhusu ikama ya wafanyakazi wa hifadhi, ilielezwa kuwa imepungua, lakini hatua zinachukuliwa kuhakikisha kuwa pengo hilo linazibwa mapema.

No comments: